Sura 6 · dakika 7 za kusoma
Ukweli wa Kusikitisha
Shauku ya Mungu, na jambo la kwanza moyoni mwa Yesu, ni kwamba atakuwa na watu ambao upendo wao kwa wenzao, na moyo wa kutumikiana, utakuwa ushuhuda mkubwa hivyo kwa ulimwengu huu hata wanaume na wanawake watalia kwa shauku ya kumjua Bwana wetu. Watataka kujua siri ya amani yetu, furaha yetu, na upatano wetu. Watazitazama ndoa zetu, nyumba zetu, watoto wetu, na sehemu zetu za kazi, si kwa kutaka kulaumu, bali ili kujua siri zetu.
Baada ya kuwahimiza wasomaji wake “kujazwa Roho,” na kueleza kwamba mojawapo ya ushahidi wa kujazwa hivyo ni “kunyenyekeana katika kumcha Kristo” (Waefeso 5:21), Paulo anatoa mifano ya jinsi jambo hili linavyopaswa kuwa katika mahusiano yetu.
Ndoa ya Kikristo → Waefeso 5:22-33 Kama ndoa za Kikristo zingekuwa kama zinavyopaswa kuwa, pande zote mbili zikiwa zimejazwa Roho na kunyenyekeana, kila mmoja akimheshimu na kumpendelea mwenzake, zingekuwa ile siri iliyofunuliwa kwa ulimwengu unaotazama. Wanaume wangeuona uhusiano alionao Yesu na bibi-arusi wake, yaani kanisa, nao wangevutwa kumjua yeye kuwa msingi wa ndoa yao pia. Kungekuwa na msululu wa watu wanaotafuta wakija mlangoni mwa nyumba zetu au kanisa letu, badala ya kukimbilia, kama wafanyavyo sasa, katika mahakama za talaka!
Wanawake wangetamani kuwaheshimu waume wao wenyewe zaidi ya wanaume wengine wote, kwa sababu ya upendo wanaoupokea, nao wanaume wangetamani kuwapenda wake zao kwa sababu ya heshima wanayoipokea.
Badala ya mzunguko mbaya wa udhalimu na kulipiza kisasi ulioenea sana ulimwenguni, kungekuwa na mzunguko mtamu wa kubarikiana katika Kristo.
Ni jambo la kusikitisha sana kwamba talaka imeenea hivyo miongoni mwa waumini wa Kikristo. Huo ni ushuhuda wa namna gani?
Nyumba ya Kikristo → Waefeso 6:1-4 Pale wazazi walipo katika mahusiano sahihi na Bwana na kila mmoja na mwenzake, watoto wao hukua katika nyumba yenye usalama na upendo. Sehemu kubwa ya ushauri ninaoutoa nikiwa mchungaji unahusu majeraha waliyoyapata watoto waliokulia katika hali tofauti kabisa, ingawa mara nyingi baba “Wakristo” hushindwa kuwafundisha (au kuwarudi) watoto wao, na badala yake huwachokoza hata wakakasirika (Wakolosai 3:21).
Washauri wa Kikristo leo huzungumza kuhusu familia zilizovurugika ambapo “birika la upendo” la mtoto halijazwi kwa upendo aliooumbiwa kuupokea, kwa sababu wazazi waliovurugika hawana uwezo wa kutoa upendo huo. Mtoto haupokei upendo ambao tunda lake ni usalama, utambulisho, kujithamini, kukubalika, na kutiwa moyo. Mtoto haupokei upendo ambao tunda lake ni usalama, utambulisho, kujithamini, kukubalika, na kutiwa moyo.
Badala ya kukua wakiwa na afya njema kihisia na kiroho, huwa kama wazazi wao hasa, waliovurugika. Kamwe hawajifunzi kutembea wima katika ulimwengu wa mabega yaliyoinama na mioyo iliyovunjika. Nafasi tupu iliyo katika birika lao la upendo hujazwa na kitu kimoja: hasira, ambayo huzaa maisha ya kuyaasi makusudi ya Mungu. Watoto kama hao kamwe hawajifunzi kuwatii wazazi wao katika Bwana.
“Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakavunjika moyo” (Wakolosai 3:21).
Ni jambo la kusikitisha sana kwamba watoto wengi waasi ni matokeo ya nyumba “za Kikristo.” Huo ni ushuhuda wa namna gani?
Mahali pa Kazi → Waefeso 6:5-9 Muumini aliyejazwa Roho ameitwa kuwa shahidi mahali pake pa kazi kwa kuonyesha moyo wa mtumishi mbele ya wafanyakazi wenzake na waajiri wake, tena anapaswa kuwa mwaminifu ili kufanya kazi yake vizuri.
Ninamfahamu mwalimu ambaye shule yake ilikuwa iunganishwe na shule nyingine mbili katika mpango mkubwa wa kupanga upya. Walimu wote kutoka shule hizo tatu walikusanyika pamoja kuunda Chama cha Wafanyakazi ili kuzungumza kwa niaba ya walimu mbele ya Wasimamizi wa Shule, wakieleza matakwa yao kuhusu muundo wa majengo mapya ya shule na masharti ya ajira yao.
Mtu mmoja alipendekezwa na kuungwa mkono kwa nafasi ya urais wa chama hiki kipya. Mwingine akapendekezwa na kuungwa mkono. Kisha, kwa mshangao wake mkubwa, rafiki yangu akapendekezwa. Mara moja, wale wawili waliokuwa wamependekezwa waliondoa majina yao ili wauunge mkono uteuzi wa rafiki yangu. Hakuna jina jingine lililotolewa, naye akachaguliwa kwa kauli moja kuwawakilisha wafanyakazi wote. Alipokuwa akitoka chumbani alionyesha mshangao wake kwa mwenzake. “Ngoja tu nimwambie mke wangu,” akasema. “Hataniamini kamwe!” “Kwa nini asikuamini?” akajibu mwenzake, “Sote tunajua wewe ndiye pekee tunayeweza kumtegemea kusema kweli daima!”
Rafiki yangu ndiye alikuwa Mkristo pekee miongoni mwa wafanyakazi wakuu wa shule hizo.
Kwa masikitiko, mara nyingi huambiwa na wafanyabiashara (wakiwemo Wakristo) kwamba watu wabaya kuliko wote kufanya nao biashara ni Wakristo.
Wanataka kupata kutoka kwako kadiri iwezekanavyo kwa malipo kidogo kabisa. Ndio wabaya kuliko wote katika kutoa bakshishi, na mara nyingi ndio wa mwisho kulipa madeni! Bila shaka, huenda ikawa tunahukumiwa kwa ukali zaidi na ulimwengu kuliko wasioamini, lakini hilo linatarajiwa!
Tumeitwa kuwa na moyo wa watumishi. Tunapaswa kuishi katika kiwango cha juu zaidi cha kujitoa na ufundi wa kazi kuliko ulimwengu! Kwa masikitiko, sote twawajua waajiri na wafanyakazi Wakristo ambao hawaonyeshi maadili ya kazi yaliyojazwa Roho wala uhusiano mwema na wenzao. Huo ni ushuhuda wa namna gani?
Kupungua kwa Wafanyakazi Tafiti nyingi zinazohusika zinaonyesha kwamba sababu kuu ya wamisionari kuacha kazi ya utumishi ni mahusiano mabaya baina ya watu! Wamesoma kwa miaka mingi katika Shule za Biblia na semina za lugha, wamefanya mafunzo kwa vitendo katika makanisa ya nyumbani, wamewekeza sehemu kubwa ya maisha yao katika maandalizi, na, baada ya kipindi kimoja tu ng’ambo, wamerudi nyumbani wakiwa na uchungu, waliovunjika moyo, waliotahayari, na waliojeruhiwa. Haipaswi kuwa hivi!
Katika Amerika ya Kaskazini, wastani wa muda wa mchungaji kudumu katika kanisa la mahali ni chini ya miaka mitano. Mwaka wa kwanza ni wa fungate, wa pili ni wa kuzoeana. Katika mwaka wa tatu, kukatishwa tamaa huanza pamoja na manung’uniko ya kutoridhika; mchungaji na waumini wa kanisa wote wana matarajio yasiyotimizwa kila mmoja kwa mwenzake.
Mwaka wa nne huona kutoridhika kukija juu, mara nyingi pamoja na uchungu na mashtaka. Watu huchukua pande, joto jingi huzuka, naye mchungaji huondoka, mara nyingi akisema, “Sina sababu ya kuvumilia haya!” Huo ni ushuhuda wa namna gani?
Migogoro Kanisani Je, umewahi kuhusika katika mgogoro wa kanisa? Si jambo la kupendeza! Ninajua kanisa moja, ambalo zamani lilikuwa na zaidi ya watu mia tatu, sasa halipo tena. Kila mtu katika mji ule anaonekana kujua sehemu fulani ya hadithi hiyo, na wako watu wengi, waliokuwa waaminifu katika kuhudhuria, wanaosema kwamba kamwe hawatahudhuria kanisa tena!
Majeraha ni ya kweli kwa sababu ugomvi ulikuwa mchungu. Waumini walikuwa wakifyatuliana “risasi” wakiuana, sauti yake ikienea mji mzima. Shetani alifurahia kwa dhihaka, naye Bwana akalia!
Bila shaka, ugomvi wetu mwingi hufichwa ndani, au ni wa siri zaidi. Nilisoma makala ya kuvutia gazetini iliyoeleza juu ya kikundi cha wahudumu waliokuwa wakianzisha vikundi vya kusaidia wachungaji waliokuwa na malalamiko dhidi ya kanisa lao au shirika lao la kanisa. Ilieleza juu ya wahudumu katika dhehebu moja, waliokuwa “wakishtaki ili kupata fedha nyingi,” kisha ikaongeza kwamba makanisa ni wakatili zaidi sana kwa wachungaji wao kuliko biashara zilivyo kwa wafanyakazi wao, na kwamba walio wakali kuliko wote wako katika mapokeo ya kiinjilisti (Christian Week (Kanada), Juni 21, 94).
Tazama matangazo ya makanisa ya jioni ya Jumamosi katika gazeti lako la mtaa ili uone jinsi tunavyoshindana sisi kwa sisi katika uwanja wa kuvuta watu wengi zaidi katika kanisa letu - mara nyingi kutoka kanisa lingine! Imethibitishwa vyema kwamba ukuaji mwingi wa makanisa ni ukuaji wa kuhamia, si ukuaji wa watu kuongoka. Kusimulia mambo binafsi si jambo la kusifiwa, lakini wakati mmoja nilikuwa na tukio la kuvutia linalostahili kusimuliwa.
Ilikuwa mwanzoni mwa mwaka wa chuo kikuu, na wachungaji wote wa mahali pale walialikwa kukutana na wanafunzi ili kuwaeleza kuhusu makanisa yetu. Kila mmoja wetu alipewa dakika mbili kutoa maelezo yake.
Nilisikiliza huku, mmoja baada ya mwingine, wachungaji wakisifu fahari za makanisa yao. “Tuna ‘Kikundi cha Wanafunzi wa Chuo na Wafanyakazi’ cha ajabu, na tunaweza kutuma basi letu kukuchukua.” “Utaifurahia kweli muziki wetu - una mahadhi ya kusisimua, kama vile vijana wapendavyo!”
“Wanafunzi wenzenu wengi huhudhuria kanisa letu kwa kuwa tuko karibu na chuo.” Mimi nilikuwa takribani mchungaji wa 30 katika mstari ule, na nilikuwa nikichunga kazi ndogo iliyokuwa ikihangaika. Niliposimama, niliwaambia wanafunzi kwamba tulikuwa kanisa dogo lisilo na programu maalum. Hatukuwa na kitu cha kuwapa, isipokuwa kazi kama walitaka kutusaidia kuufikia mtaa wetu kwa ajili ya Kristo.
Nikaketi - nao wanafunzi wakaanza kupiga makofi!
Kanisa lilipokua, idadi kubwa ya waumini wetu walikuwa wanafunzi wa chuo kikuu. Kwa nini tushindane sisi kwa sisi kwa ajili ya kondoo hali sote tunamtumikia Mchungaji Mkuu yuleyule? Huo ni ushuhuda wa namna gani?
Kwa nini tunaona ni vigumu hivyo kuheshimiana, kupendana, na kutumikiana? Je, ni kiburi chetu tu kinachozuia njia, huku wakati huohuo tukizungumza juu ya kujazwa Roho? Au sisi ni wajinga tu wa ukweli kwamba tuko vitani, na kwamba adui ni mwerevu sana?
Uwe na hakika kabisa na hili! Kama ni jambo la kwanza kwa Bwana kuwa na watu walio katika mahusiano sahihi kila mmoja na mwenzake kwa kulitii Neno lake, bila shaka ni jambo la kwanza kwa Shetani kuharibu mahusiano kama hayo! “Gawanya na utawale,” yaweza kabisa kuwa kauli yake ya mbiu.