Sura 33 · dakika 5 za kusoma

Yeye Peke Yake

Basi Yesu, hali akijua ya kuwa wangekuja kumshika ili wamfanye mfalme kwa nguvu, akajitenga tena akaenda mlimani yeye peke yake.” Yohana 6: 15.

Injili mara nyingi hutuambia juu ya Kristo kwenda faraghani ili kuomba. Luka hutaja kuomba kwake mara kumi na moja. Marko hutuambia katika sura yake ya kwanza kabisa, ya kuwa baada ya jioni ambapo mji wote ulikuwa umekusanyika mlangoni, naye alikuwa amewaponya wengi, “Hata alfajiri na mapema sana akaondoka akatoka, akaenda zake mahali pasipokuwa na watu, akaomba huko.” Kabla ya kuwachagua mitume wake kumi na wawili “Siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu.” Wazo hili la kujitenga kabisa laonekana liliwavutia sana wanafunzi, likizaa matumizi ya Yohana ya usemi wenye maana, “Yesu akajitenga tena akaenda mlimani yeye peke yake.” kama vile Mathayo naye alivyokuwa ameandika, “Akapanda mlimani faraghani ili kuomba. Kulipokuwa jioni alikuwako huko peke yake” Kristo alihisi hitaji la faragha kamili. Na tutafute kwa unyenyekevu kupata maana ya hili.

1. Yeye peke yake. Akiwa peke yake kabisa, peke yake na nafsi yake. Twajua ni kwa kiasi gani umoja na wanadamu hutuvuta mbali na nafsi zetu na kuchosha nguvu zetu. Yesu, mtu, alijua hili pia naye alihisi hitaji la kujirudia mwenyewe, la kuzikusanya nguvu zake zote au kufanya upya fahamu ya alichokuwa na alichokihitaji, la kutambua kikamilifu kusudi lake tukufu, udhaifu wake wa kibinadamu, na kutegemea kwake kote kwa Baba. Ni kwa kiasi gani zaidi mtoto wa Mungu ahitaji hili? Ikiwa ni katikati ya kukengeushwa kwa shughuli za kidunia au huduma ya kidini, ikiwa ni kwa ajili ya kudumisha maisha yetu wenyewe ya Kikristo au kufanya upya nguvu yetu ya kuwavuta wanadamu kwa Mungu, kuna daima wito wa dharura kwa kila mwamini kufuata katika nyayo za Bwana wake na kupata mahali na wakati ambapo aweza kweli kuwa na nafsi yake peke yake.

2. Yeye peke yake, pamoja na hali halisi za kiroho. Ni katika kujitenga kabisa na kugusana na vitu vinavyoonekana na vya muda ndipo tulipo huru kujitoa kikamilifu kwa nguvu za ulimwengu usioonekana na kuziacha zitutawale. Yesu alihitaji wakati na utulivu upya daima ili kutambua nguvu ya ufalme wa giza aliokuja kupambana nao na kuushinda, hitaji la ulimwengu huu mkubwa wa wanadamu aliokuja kuuokoa, uwepo na nguvu ya Baba ambaye alikuja kuyatenda mapenzi yake. Hakuna kilicho cha lazima zaidi katika huduma ya Kikristo kuliko ya kuwa mtu ajiweke nyakati fulani kufikiri kwa nguvu juu ya hali halisi za kiroho ambazo, kama jambo la ujuzi, amezizoea sana, na ambazo hata hivyo mara nyingi hutumia nguvu ndogo sana juu ya moyo na maisha.

Kweli za umilele zina nguvu isiyo na kikomo; mara nyingi hazina nguvu hivyo kwa sababu hatuzipi wakati wa kujifunua zenyewe. Yeye peke yake — hii ndiyo tiba pekee.

3. Yeye peke yake, pamoja na Mungu Baba. Hunenwa ya kuwa kazi ni ibada, ya kuwa huduma ni ushirika. Kama kuwapo mtu awezaye kujiepusha na nyakati za pekee za faragha na ushirika, alikuwa Bwana wetu aliyebarikiwa. Lakini hangeweza kufanya kazi yake au kudumisha ushirika wake katika nguvu kamili, pasipo wakati wake wa utulivu. Alihisi hitaji kama mtu la kuleta kazi yake yote, ya wakati uliopita na ujao, na kuiweka mbele za Baba, la kufanya upya fahamu yake ya kutegemea kabisa upendo wa Baba, katika nyakati za ushirika wa pekee. Aliposema: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe,” kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo,” alikuwa akieleza tu kweli rahisi ya uhusiano wake na Mungu; ni hili lililofanya kujitenga kwake kuwa jambo la lazima na furaha isiyoelezeka. Mungu angejalia ya kuwa kila mtumishi wake angeelewa na kutenda ustadi huu uliobarikiwa, na ya kuwa Kanisa lingejua jinsi ya kuwazoeza watoto wake kuwa na fahamu fulani ya pendeleo hili tukufu na takatifu, ya kuwa kila mwamini aweza na yampasa kuwa na wakati wake ambapo yeye kwa kweli ni — yeye peke yake na Mungu. Ee! Wazo la kuwa na Mungu peke yangu kabisa kwa nafsi yangu, na kujua ya kuwa Mungu ananimiliki peke yangu kabisa kwake mwenyewe.

4. Yeye peke yake, pamoja na Neno. Kama mtu Bwana wetu ilimpasa kujifunza Neno la Mungu akiwa mtoto; katika miaka mingi ya maisha yake huko Nazareti, alilishwa na Neno hilo na kulifanya kuwa lake mwenyewe. Katika faragha yake, alishauriana na Baba juu ya yote ambayo Neno hilo lilisema juu yake, juu ya mapenzi yote ya Mungu aliyoyafunua ili ayatende. Katika maisha ya Mkristo, ni mojawapo ya mafunzo yaliyo ya kina zaidi ayapaswayo kujifunza, ya kuwa Neno pasipo Mungu aliye hai lafaa kidogo; ya kuwa baraka ya Neno huja pale linapotuleta kwa Mungu aliye hai; ya kuwa Neno tulipatalo kutoka katika kinywa cha Mungu huleta nguvu ya kulijua na kulitenda.

Na tujifunze funzo hili: ushirika binafsi na Mungu sirini peke yake ndio uwezao kufanya neno kuwa uzima na nguvu.

5. Yeye peke yake, katika maombi. Ni pendeleo lisiloelezeka jinsi gani maombi kwa jinsi linavyomruhusu mtu kuweka wazi maisha yake yote mbele za Mungu, na kuomba fundisho lake na nguvu yake. Jaribu tu kwa muda kufikiri maana ya maombi kwa Yesu, ni ibada ya kuabudu ilioje, upendo wa unyenyekevu ulioje, kusihi kama kwa mtoto kulikoje kwa yote aliyoyahitaji. Kama vile tuwezavyo kidogo kuwaza hili ipasavyo, ndivyo tuwezavyo kutambua heri iliojemngojeayo mtu ajuaye kufuata katika nyayo za Kristo, na kuthibitisha ni nini kilicho cha juu kabisa Mungu awezacho kumtendea mtu afanyaye hili kuwa furaha yake kuu — kuwa naye, yeye peke yake?

Yeye peke yake. Ni kwa kina jinsi gani maneno haya hutufunulia siri ya maisha ya Kristo duniani, na ya maisha ambayo sasa aishi ndani yetu. Ya maisha aishiyo ndani yetu kwa Roho wake Mtakatifu, hiki ni mojawapo ya vipengele vilivyobarikiwa zaidi, ya kuwa hutufunulia na kututia ndani yale yote ambayo Neno lamaanisha — yeye peke yake.

Ukurasa 1 / 4 · 5 dakika zimebaki katika sura
Ochorus

Kuwawezesha watu vitabu vya Kikristo vya kale — bila malipo, kwa lugha yako.

Chunguza

Dhamira Yetu

Vitabu vya Kikristo vya kale bila malipo mtandaoni — na vitabu vilivyochapishwa tunavyogawa kwenye makongamano, makanisa, shule na magereza kote Afrika Mashariki.

Faragha na Masharti

Huduma tangu 2021 · Victoria BC, Kanada · Kampala, Uganda