Sura 32 · dakika 5 za kusoma
Ndani ya Kristo
Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu, kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Yohana 15: 4.
Fundisho lote hutokea kutoka ya nje kuelekea ya ndani. Baadhi ya ujuzi wa hali halisi ukiisha kupatikana, katika maneno au matendo, katika asili au historia, akili huandaliwa kutafuta maana ya ndani iliyofichwa ndani yavyo. Ni vivyo hivyo na fundisho la maandiko kuhusu Yesu Kristo. Anawekwa mbele yetu kama mtu miongoni mwetu, mbele yetu, juu yetu, akifanya kazi kwa ajili yetu hapa duniani, akiendeleza kazi hiyo kwa ajili yetu bado huko mbinguni.
Wakristo wengi hawaendi mbele zaidi ya hili, Bwana wa nje aliyeinuliwa, wanayemtumaini kwa yale aliyoyafanya na ayafanyayo kwa ajili yao na ndani yao. Wanajua na kufurahia kidogo tu ya nguvu ya siri ya kweli ya Kristo ndani yetu, ya uwepo wake wa ndani, kama Mwokozi akaaye ndani. Mtazamo wa kwanza na rahisi zaidi ni ule wa Injili tatu za kwanza; wa mwisho hutia alama Injili ya Yohana. Wa kwanza ni upande wa kweli uwasilishwao katika fundisho la Maandiko la kuhesabiwa haki. Wa mwisho ni fundisho kuhusu muungano wa mwamini na Kristo na kukaa kwake kwa daima, kama lifundishwavyo hasa katika Yohana na Nyaraka za kwa Waefeso na Wakolosai.
Kwa Wakristo ambao kitabu hiki kimeandikwa kwa ajili yao na ambao wote yawapasa kuwa wanajiandaa kumpeleka Kristo kwa wenzao, siwezi kusema kwa bidii ya kutosha: Angalia ya kuwa kukaa huku ndani ya Kristo na Kristo ndani yako kusiwe tu kweli uishikayo katika nafasi yake ipasayo katika mpango wako wa fundisho la Injili bali ya kuwa, kama jambo la uzima na uzoefu, kunahuisha imani yako yote katika Kristo na umoja na Mungu. Kuwa ndani ya chumba kwamaanisha kuwa na vyote vilivyomo humo tayari kwa matumizi yako, samani zake, faraja zake, mianga yake, hewa yake, kivuli chake. Kuwa ndani ya Kristo, kukaa ndani ya Kristo, na kujua maana yake. Si jambo la imani au dhana ya kiakili, bali hali halisi ya kiroho.
Fikiri juu ya nani na nini Kristo alivyo. Mfikiri katika hali au hatua tano zitiazo alama na kufunua asili yake na kazi yake. Yeye ni yeye aliyefanyika mwili, ambaye ndani yake twaona jinsi Uweza wa Mungu ulivyounganisha kwa ukamilifu asili ya Kimungu na ya kibinadamu. Tukiishi ndani yake twashiriki asili ya Kimungu, na uzima wa milele. Yeye ni yeye Mtii, akiishi maisha ya kujisalimisha kote kwa Mungu na kutegemea kikamilifu kwake. Tukiishi ndani yake maisha yetu huwa ya kunyenyekea kabisa mapenzi ya Mungu, na kungoja daima uongozi wake. Yeye ni yeye Aliyesulubiwa, aliyeifia dhambi na kuifia dhambi ili apate kuiondoa. Tukiishi ndani yake tu huru kutoka katika laana yake na utawala wake, nasi twaishi, kama yeye, katika kufa kwa ulimwengu na kwa mapenzi yetu wenyewe. Yeye ni yeye Aliyefufuka, aishiye hata milele.
Tukiishi ndani yake twashiriki nguvu yake ya ufufuo na kuenenda katika upya wa uzima, uzima uliozishinda dhambi na mauti.
Yeye ni yeye Aliyeinuliwa, aketiye juu ya kiti cha enzi na kuendeleza kazi yake kwa ajili ya wokovu wa wanadamu. Tukiishi ndani yake upendo wake hutumiliki, nasi twajitoa kwake atutumie katika kuurudisha ulimwengu kwa Mungu. Kuwa ndani ya Kristo, kukaa ndani yake, kwamaanisha kisicho pungufu ya nafsi kuwekwa na Mungu mwenyewe katikati ya mazingira haya ya ajabu ya uzima wa Kristo ambao ni wa kibinadamu na wa Kimungu kwa pamoja, uliojitoa kabisa kwa Mungu, katika utii na dhabihu, uliojaa Mungu kabisa katika uzima wa ufufuo na utukufu. Asili na sifa ya Yesu Kristo — tabia zake na mapendo yake, nguvu yake na utukufu wake — hivi ndivyo vipengele tunavyoishi ndani yavyo, hewa tuipumuayo, uzima ambamo uzima wetu wakaa na kukua.
Dhihirisho kamili la Mungu na upendo wake wa kuokoa laweza kuja kwa namna nyingine yoyote isipokuwa kwa kukaa ndani. Kwa uwezo wa Uungu wa Kristo na nguvu ya Kimungu, aweza, kadiri tu tukaavyo ndani yake, kukaa ndani yetu. Kadiri moyo pamoja na upendo wake utolewavyo kwake kwa imani, na utashi katika utii wa vitendo, huingia na kufanya makao ndani yetu. Twaweza kusema kwa sababu twajua — Kristo aishi ndani yangu.
Na sasa, ili kufikia lengo letu kuu, kama uzima huu, Kristo ndani yetu na sisi ndani yake, utakuwa maisha yetu halisi ya siku ya kazi, roho yake ni lazima ifanywe upya na kutiwa nguvu katika umoja binafsi na Mungu ambao kwao twaanza siku katika saa ya kesha ya asubuhi.
Njia yetu ya kumfikia Mungu, dhabihu yetu kwa Mungu, na matarajio yetu kutoka kwa Mungu ni lazima yote yawe ndani ya Kristo, katika ushirika ulio hai naye.
Kamwe uhisipo ya kuwa wataka kumkaribia Mungu zaidi, kutambua uwepo wake au nguvu yake, au upendo, au mapenzi, au kutenda kazi kwake, kwa ukamilifu zaidi, kwa neno moja kuwa na Mungu zaidi — mwendee Mungu ndani ya Kristo. Fikiri jinsi, kama mtu duniani, alivyomkaribia Baba katika unyenyekevu wa kina na kutegemea, katika kujisalimisha kote na utii kamili, na uje katika Roho yake na tabia yake, katika muungano naye. Tafuta kuchukua nafasi ile ile mbele za Mungu ambayo Kristo ameichukua mbinguni ile ya ukombozi uliotimizwa, ya ushindi mkamilifu, ya kuingia kamili katika utukufu wa Mungu.
Chukua nafasi ile ile mbele za Mungu ambayo Kristo aliichukua duniani katika njia yake ya kwenda kwenye ushindi na utukufu. Ifanye katika imani ya kukaa kwake ndani na nguvu yake ya kukuwezesha ndani yako hapa duniani; tegemea kwa uthabiti ya kuwa kumkaribia kwako kunakubaliwa si kwa kadiri ya kufikia kwako, bali kwa kadiri ya unyofu wa kujisalimisha kwa moyo wako, na ukamilifu wa kukubaliwa kwako ndani ya Kristo, nawe utaongozwa mbele katika njia ambamo, Kristo akiishi ndani yako na kunena ndani yako, kutakuwa kweli na nguvu.