Sura 4 · dakika 10 za kusoma
Kuenenda kwa Imani
Ikiwa ungechagua baadhi ya wahusika wa Biblia ili kuonyesha maana ya kuenenda kwa imani, ungewachagua akina nani?
Je, Kalebu, ambaye ingawa alikuwa na umri wa zaidi ya miaka themanini, alitaka kupigana na majitu? Au Elisha, aliyesimama kupinga manabii wote wa Baali?
Au Danieli, aliyeomba hadharani akijua kwamba huenda ikamgharimu maisha yake? Lakini inavutia kuona ni akina nani ambao Biblia inawataja kuwa mifano ya imani.
Hakuna hata mmoja kati ya hao!
Mtume Paulo anaandika kuhusu imani katika waraka wake kwa Warumi akitangaza, “Kwa hiyo twaona ya kuwa mwanadamu huhesabiwa haki kwa imani pasipo matendo ya sheria” (Warumi 3:28). Kisha anatumia sura yote ya nne kutoa mfano wake wa baba wa taifa Ibrahimu, ambaye ‘imani yake ilihesabiwa kuwa haki.’
Mtume Yakobo pia anamchukua Ibrahimu kuwa mfano wake mkuu wa maisha ya imani, akitangaza kwamba imani pasipo matendo imekufa.
Anauliza, “Je! Ibrahimu, baba yetu, hakuhesabiwa haki kwa matendo, hapo alipomtoa Isaka mwanawe juu ya madhabahu? Waona kwamba imani ilitenda kazi pamoja na matendo yake, na kwa matendo hiyo imani ikakamilishwa” (Yakobo 2:21-22).
Hata hivyo, Yakobo anaongeza mfano wa pili, ambao lazima uonekane wa ajabu kwetu sote. Anatuletea Rahabu kahaba, aliyewakaribisha wapelelezi waliotumwa ndani ya Yeriko. Kwa vipimo vyote vya kibinadamu, hakuwa mtu wa kusifiwa hata kidogo; zaidi ya kufuata biashara ya kudharauliwa, alikuwa msaliti na mwongo aliyejali usalama wake mwenyewe tu. Lakini anatajwa kuwa mfano wa imani.
Kinachoshangaza zaidi ni kwamba Yakobo si peke yake anayemwona hivyo! Mwandishi wa Waebrania pia anamtaja katika orodha yake ndefu. Katika uelewa wangu wa awali wa imani, hakika nisingemhesabu yeye, wala wengine wengi wanaotajwa katika Waebrania 11! Basi, huenda ni uelewa wangu wa imani ndio unaopaswa kubadilika.
Wengine hata wangeliita Waebrania 11 “Mashujaa wa Imani.” Mimi sioni mashujaa humo. Ni watu wa kawaida tu kama wewe na mimi walioyapitia kila aina ya mazingira katika kuenenda kwa imani.
Wengine walishinda milki kwa imani, hali wengine waliuawa kwa imani! Kichwa bora zaidi kwa sura hii kingekuwa “Mifano ya Imani,” kwa kuwa lengo lake ni kutuonyesha kwamba, katika enzi yake kuu, Mungu huwaongoza wanaume na wanawake katika njia nyingi tofauti ili kutimiza mapenzi yake ndani yao na kupitia kwao.
Kwetu sisi, mateso na kifo havionekani kupatana na mapenzi ya Mungu kwa mwamini, lakini historia imejaa hadithi za jinsi kanisa lilivyokua kwa kasi juu ya damu ya mashahidi. Yalikuwa mapenzi ya Mungu kwamba wafe, ili wapate kuwa ‘sifa ya utukufu wake.’ Hii haimaanishi kwamba yeye hana huruma juu ya hisia za watu.
Bila shaka anayo, lakini, miongoni mwa watakatifu wake, anawakuza wale ambao, kwa mateso na kifo chao, watamletea utukufu mkuu zaidi kuliko kwa maisha yao. Kwao amehakikisha ‘ufufuo ulio bora zaidi.’
Nyakati nyingine juu ya mlima ambapo jua huangaza sana, Mungu huwaongoza watoto wake wapendwa.
Nyakati nyingine bondeni, katika giza nene la usiku, Mungu huwaongoza watoto wake wapendwa.
Wengine kupitia majini, wengine kupitia gharika, Wengine kupitia motoni, lakini wote kupitia damu.
Wengine kupitia huzuni kuu, lakini Mungu hutoa wimbo, Wakati wa usiku na mchana kutwa” (G.A Young).
Katika Injili tunasoma juu ya watu sita tu ambao Yesu aliwasifu kwa imani yao. Ikiwa machaguo ya Paulo, Yakobo na mwandishi wa Waebrania yanakushangaza, ngoja hadi uwaone wale ambao Yesu anawachagua!
Angalau watatu kati yao hawakuwa hata Wayahudi, mmoja alikuwa mkoma, mwingine alikuwa mgonjwa kwa miaka mingi, mmoja alikuwa kipofu, watatu walijitangaza kuwa ‘hawastahili’ na wote walikuwa wenye dhambi.
Akida wa Kirumi → Mathayo 8:5-13 Mtumishi wake alikuwa amelala nyumbani amepooza, hivyo alimwomba Bwana kama angemponya.
“Nitakuja kwako,” akasema Bwana, lakini yule akida akamjibu, “Bwana, mimi sistahili wewe uingie chini ya dari yangu, lakini nena neno tu na mtumishi wangu atapona!”
Na tuelewe hili; huenda alikuwa na nyumba iliyo bora zaidi mjini, kwa kuwa cheo cha akida katika jeshi la Kirumi kilikuwa cha heshima kubwa. Kutostahili kwake hakukutokana na hadhi yake, bali kwa sababu alitambua kwamba alikuwa mbele ya mtu aliye mkuu zaidi kuliko yeye mwenyewe. Aliendelea, “Bwana, mimi ni kama wewe, mtu niliye chini ya mamlaka.”
Yesu alimwona kuwa chini ya mamlaka gani? Hakuwa na mamlaka aliyokabidhiwa na wenye mamlaka wa Kiyahudi, wala hakuwa na hadhi ya mtu aliyefundishwa miguuni pa rabi mkuu. Alikuwa seremala wa hali ya chini, lakini alikuwa na mamlaka ya upako wa Mungu, na yule akida alitambua hili. Jinsi gani? Kwa imani!
Yesu alistaajabu na kusema, “Sijaona imani kubwa namna hii katika Israeli yote!”
Imani ilikuwa wapi? Yule akida alikuwa na ushuhuda wa ndani kwamba mtu huyu, Yesu, alikuwa mtu mwenye mamlaka ya kimungu. Aliutii ushuhuda huo (wa Roho Mtakatifu) na akajisalimisha chini ya mamlaka hiyo.
“‘Bwana, sistahili wewe kuingia chini ya dari yangu; lakini nena neno tu, na mtumishi wangu atapona’” (Mathayo 8:8).
Mwanamke Aliyekuwa na Kutokwa na Damu → Marko 5:25-34 Mwanamke huyu mwenye bahati mbaya alikuwa ameteseka sana mikononi mwa waganga wengi bila kupata uponyaji wa hali yake ya aibu na dhiki. Naam, alikuwa akizidi kuwa mbaya zaidi.
Sheria ilimtangaza kuwa ‘najisi’ hivyo hakuruhusiwa kufurahia mengi ya mapendeleo ya watu wa kawaida. Hakuweza kuhudhuria sherehe za Siku za Sikukuu, wala kuingia sinagogi kuabudu, na zaidi ya yote, hakupaswa kuwakaribia Mafarisayo ‘wenye haki’ na ‘watu watakatifu.’
Alikuwa amesikia habari za Yesu, lakini ushuhuda wa ndani ulimwambia anyoshe mkono kugusa upindo wa vazi lake. Hili lilikuwa kinyume na kila kitu alichokuwa amefundishwa, lakini alitii na akaponywa. Hapakuwa na mfano wa jambo kama hili uliotangulia. Hakuamini kwa sababu alikuwa amesikia juu ya wengine walioponywa kwa njia iyo hiyo.
Alitii tu msukumo wa ndani.
“Naye akamwambia, ‘Binti, imani yako imekuponya; enenda zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na ugonjwa wako tena’” (Marko 5:34).
Mwanamke Mkanaani → Mathayo 15:22-28 Moyo wa mwanamke huyu ulikuwa unavunjika alipokuwa akitafuta msaada kwa ajili ya binti yake aliyepagawa na pepo. Alikuja kwa Bwana, lakini hata yeye alionekana kumkwepa na wanafunzi wake wakajaribu kumfukuza.
Hakuwa Myahudi, lakini aliona kile ambacho karibu hakuna mtu mwingine aliyekuwa amekiona, hata wanafunzi hadi wakati huo. Alimtambua Yesu kuwa Bwana, Mwana wa Daudi. Haya yalikuwa maneno yaliyofahamika vyema kumhusu Masihi ajaye. Wengine walikuwa bado hawajamtambua, lakini mwanamke huyu Mkanaani alikuwa amemtambua. Ufunuo kama huo huja tu kwa ushuhuda wa ndani wa Roho Mtakatifu. Ufunuo huohuo ulimjia Petro juu ya Mlima Hermoni karibu miaka miwili baadaye!
Yesu aliujaribu uelewa wake, ufunuo wake, kwa kumpinga kwamba haikuwa vyema kutupa mkate wa watoto (uponyaji kwa Wayahudi) kwa mbwa (Mataifa). Jibu lake linaonyesha kwamba alielewa kikamilifu, kwa ufunuo, kwamba kweli alikuwa Masihi.
“Ndipo Yesu akajibu, akamwambia, ‘Mama, imani yako ni kubwa; na ufanyiwe kama utakavyo.’ Akapona binti yake tangu saa ile” (Mathayo 15:28).
Bartimayo Kipofu → Marko 10:46-52 Ingawa alikuwa kipofu, Bartimayo aliweza kuona zaidi ya ule umati mkubwa wa watu wenye kuona waliomzunguka Yesu. Aliishi katika mji uliolaaniwa wa Yeriko na alikuwa amepoteza kuona kwake, akawa ombaomba, aliyedharauliwa na wote waliomzunguka. Alipopiga kelele watu walimwamuru kwa ukali anyamaze, lakini hakuacha kupiga kelele, kwa kuwa kama yule mwanamke Mkanaani, alikuwa amepokea ufunuo, ushuhuda wa ndani wa Yesu kuwa Masihi. “Akapaza sauti… ‘Mwana wa Daudi, Yesu, unirehemu’” (Marko 10:48).
Yesu alimwita yule ombaomba na kumuuliza swali la ajabu, “Wataka nikufanyie nini?” Bartimayo akajibu, “Mwalimu, nataka nipate kuona!” Yesu akamwambia, “Enenda zako, imani yako imekuponya,” na mara akapata kuona (Marko 10:51-52).
Ufunuo ulikuwa umetangulia ungamo, na uponyaji ukawa matokeo yake.
Mwanamke Katika Nyumba ya Simoni → Luka 7:37-50 Katika Yohana 11:2 na Mathayo 26:6 inasemekana kwamba mwanamke huyu alikuwa Mariamu, dada yake Lazaro. Simoni, Farisayo, aliyatazama matendo yake na akaanza kumhukumu Yesu kuwa hana ufahamu, kwa kuwa mwanamke huyu alifahamika kuwa mwenye dhambi. Lakini Yesu alifahamu kikamilifu yeye alikuwa nani, naye aliyaona matendo yake kuwa yanamtayarisha kwa maziko. Huenda mwanamke huyu alikuwa na uelewa mdogo wa hili lakini, akitenda kwa kutii ushuhuda wa ndani, msukumo wa Roho Mtakatifu, na akisukumwa na upendo, alikuwa amemtumikia Bwana kwa njia ya kinabii.
“[Yesu] akamwambia yule mwanamke, ‘Imani yako imekuokoa; enenda zako kwa amani’” (Luka 7:50).
Mkoma wa Kumi → Luka 17:11-19 Wakoma kumi walikuwa wamekuja kwa Yesu wakitafuta kuponywa. Wote walitii maagizo yake ya kwenda kwa makuhani, ili watangazwe kuwa ‘safi.’ Hili lilikuwa takwa la Agano la Kale na, ingawa mmoja wao alikuwa Msamaria, yeye pia alitii. Wakiwa njiani kwenda kwa makuhani, wote waliponywa, lakini ni Msamaria peke yake aliyekiri kwamba uponyaji wake haukuwa mchezo wa kimazingaombwe, bali ulitokana na Mungu, hivyo, akianguka miguuni pa Yesu, alianza kumtukuza Mungu. Alikuwa ameitii sauti ya wazi ya Mwana wa Mungu na akaponywa.
“[Yesu] akamwambia, ‘Inuka, enenda zako; imani yako imekuponya’” (Luka 17:19).
Katika mifano yote sita, imani ilidhihirishwa na kutimizwa katika utii. Kama hapakuwa na utii kwa kutambua mamlaka, kwa ufunuo wa umungu, kwa ushuhuda wa ndani wa msukumo wa Roho, kwa neno lililonenwa la Bwana, hapangekuwa na miujiza iliyoandikwa.
Maana ya Imani Basi tutaifafanuaje imani ili ijibu maswali yote ya mabishano na kueleza machaguo ya Yesu, Paulo, Yakobo, na mwandishi wa Waebrania?
Ninapowauliza watu waifafanue imani, jibu la kawaida ni kunukuu Waebrania 11:1, “Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” lakini, wanapoombwa kueleza fasili yao, ninakuta ni wachache wenye maelezo yenye kushawishi.
Kwangu mimi, mwandishi anasema tu kile ambacho mtume Paulo amekisema mahali pengine, kama kilivyonukuliwa katika sura iliyotangulia.
Ni nini tunachokitumaini? Barclay, mwandishi wa mfululizo maarufu wa ibada, Our Daily Bread, anafafanua tumaini kuwa “kutazamia kwa hamu kile kilichoahidiwa.” Mitume Paulo na Petro wote walitoa ushuhuda mbele ya washtaki wao juu ya tumaini letu kuu la Ufufuo. Kwao, tumaini letu ni hakika. Kwa mwandishi wa Waebrania, ni kama nanga iliyokitwa ndani ya pazia la uwepo wa Mungu. Tunatumaini kile ambacho hakika tutakipokea.
Tutapokea nini, isipokuwa kile kinachotiririka kutoka neema ya Mungu; kile ambacho ameahidi? Kipawa chake cha wokovu, kipawa chake cha Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu; vipawa vyake vitolewavyo na Roho Mtakatifu: kipawa chake.
Namwazia mtoto mdogo wakati wa Krismasi au siku ya kuzaliwa. Anajua atapokea kitu maalum kutoka kwa wazazi wake - zawadi itokayo katika upendo wao. Anaingojea siku ile kuu kwa hamu. Ana tumaini kwa kile ambacho hakika kitakuja. Hatimaye, anapokea kile kilichoahidiwa: zawadi yake. Hii ndiyo hakika ya kile alichokitumaini. Matarajio yake yamekuwa uhalisia.
Imani ni hakika ya mambo yatarajiwayo; ni kipawa.
Nilipowasili Kanada kwa mara ya kwanza, niliitazama miti iliyokuwa bustanini mwetu nikitazamia kwa hamu kufurahia matunda yake majira ya kuchipua yaliyofuata; hata hivyo, sikuwa na ufahamu wa aina ya miti ile ilivyokuwa. Mimi si msomi wa kilimo cha bustani, na sikuweza kuitambua miti kwa majani au umbo lake. Lakini matunda yalipoanza kuja, sikuwa na shaka ni matunda ya aina gani kila mmoja. Niliitambua kwa matunda yake. Tunda lilikuwa ushahidi niliouhitaji.
Asili ya miti ile haikuwa imebadilika, tabia ya miti ile haikuwa imebadilika, lakini haya yalikuwa yamefichwa kutoka ufahamu wangu, hadi matunda yalipokuja. Bayana ya mambo yasiyoonekana ilikuwa ni matunda juu ya matawi.
Vivyo hivyo, bayana ya maisha yaliyojaa Roho iko katika tunda lake.
Yesu alisema, “Ufanyeni mti kuwa mzuri, na matunda yake kuwa mazuri; au ufanyeni mti kuwa mbaya, na matunda yake kuwa mabaya; kwa maana mti hutambulikana kwa matunda yake” (Mathayo 12:33) Imani ni bayana ya mambo yasiyoonekana. Ni tunda.
Mwandishi wa Waebrania 11 hasemi zaidi ya kile Paulo alichosema katika 1 Wakorintho 12:9 na Wagalatia 5:22.
Mimi naifafanua imani kuwa ni kidole cha Mungu ndani ya mioyo ya wanaume na wanawake, kikiwasukuma kufanya mapenzi yake.
Inadhihirishwa katika utii kama mwelekeo wa moyo. Si mwelekeo wa akili. Ni kuamini na kuitikia. Kidole kinachosukuma ni cha Mungu, itikio la utii ni letu. Kazi ya kwanza na kuu zaidi ya imani ambayo mtu aweza kuifanya ni kumwamini Bwana Yesu Kristo hata wokovu. Ufunuo hutangulia ungamo (ona Petro juu ya Mlima Hermoni). Inadhihirishwa katika toba, ubatizo, ungamo na matendo mema (matendo ya haki). Pale ambapo haya hayadhihiriki, mtu aweza kwa haki kutia shaka (kama Yakobo) juu ya uhalisia wa imani; kwa kweli imani hiyo ‘imekufa’ (Yakobo 2:26).
Kuenenda kwa imani ni kujisalimisha kila siku kwa mapenzi yake (yaliyofunuliwa na yasiyofunuliwa). Kushikilia mkono wa Baba! Kama Petro alivyosema, “Twende kwa nani?” (Yohana 6:68). Tunaposhikilia, Baba yetu aweza kuiondoa milima! Hii ni kwa sababu ya tabia yake, si kwa sababu ya nguvu za akili au imani yetu! Angalia kwamba hata mashetani wanaamini yote ambayo Baba yetu aweza kuyafanya, lakini hilo halihesabiwi kuwa imani (Yakobo 2:19).