Sura 3 · dakika 19 za kusoma

Aina Tatu za Imani

Ninapoichunguza Maandiko, napata aina tatu za imani: imani iokoayo, tunda la imani, kipawa cha imani.

Imani Iokoayo “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu” (Waefeso 2:8-9).

Haya ndiyo yaliyowapata wote waliozaliwa mara ya pili - waliozaliwa na Roho. Tunakiri kwamba sisi ni wenye dhambi tusio na tumaini lolote katika ulimwengu huu, tena wenye kuihitaji sana kwa dhati ya moyo Mungu aingilie kati maisha yetu. Tunakwenda gizani, tusio na haki, tena wageni kwa ahadi na baraka zake.

Kama si kwa sababu Mungu ameingia katika hali yetu ya kibinadamu na kutufunulia upendo wake kwa njia ya kifo cha Mwanawe msalabani, tungekuwa bado tumekufa katika dhambi zetu na wenye taabu kuliko wote; lakini haki ya Mungu imefunuliwa kwetu, “ni haki ya Mungu iliyo kwa njia ya imani katika Yesu Kristo kwa wote waaminio” (Warumi 3:22).

Paulo anatangaza kwamba Mungu huwahesabia haki wote walio na imani katika Yesu (Warumi 3:26). Neno hilo ni zuri jinsi gani! Kuhesabiwa haki - kana kwamba sikupata kutenda dhambi kamwe! Ndivyo Mungu anavyotutazama sasa. Anatuona ‘ndani ya Mwanawe’ wala si katika dhambi yetu. Kwanza kabisa ilikuwa ni neema yake ikifanya kazi. Alituonyesha upendeleo tusiostahili.

Naam, mojawapo ya maana nyingi za neema ni “upendeleo usiostahiliwa;” lakini maana niipendayo zaidi ni fumbo hili la herufi za mwanzo katika Kiingereza: G od’s R iches A t C hrist’s E xpense (yaani, Utajiri wa Mungu kwa Gharama ya Kristo). Alilipa gharama ili nipate kuzipokea baraka zote za maisha haya ya ajabu ya Kikristo.

Tukiwa bado katika habari ya neema, je, umewahi kufikiri tofauti iliyopo kati ya neema na rehema? Acha nikuwekee tofauti hii kwa baraka yako: Neema ni Mungu kunitendea kinyume na ninavyostahili, ambapo rehema ni Mungu kutonitendea kama ninavyostahili!

Kipawa hiki cha neema kutoka kwa Mungu ni lazima kipokewe kwa imani, ambayo nimeiita imani iokoayo; lakini hata hii ni kipawa kutoka kwa Mungu. Siwezi kuamini kwa imani isipokuwa Mungu anipe uwezo wa kufanya hivyo!

Hakuna chanzo cha imani ndani yangu. Naweza kuchagua kuamini, tena naweza kutamani kuamini, lakini uwezo wa kuitumia imani iokoayo unanipita. Naweza kuamini kichwani mwangu, lakini nahitaji kuamini moyoni mwangu, kwa kuwa jambo hilo ndilo litofautishalo kati ya wale waliohesabiwa haki na wale wangali katika dhambi zao.

Kwa muda wa miaka miwili nilipata pendeleo la kufundisha katika Chuo cha Kiyahudi. Cheo changu kilikuwa Mkuu wa Idara ya Sayansi, lakini karibu na mwisho wa kipindi changu katika shule ile, nilialikwa kuzungumza na darasa la wanafunzi wakubwa kuhusu imani ya Kikristo. Mwalimu aliyekuwa akisimamia darasa lile aliniambia kwamba walikuwa wakijifunza Dini za Kulinganisha na kwamba “somo la leo ni Ukristo!” Somo moja tu la kujifunza jambo ambalo wengi hulitumia maisha yao yote – na bado hawalielewi!

Asubuhi iliyofuata, niliombwa nimtembelee rabi mkuu, mkutano ambao sikuufurahia kwa kuwa hakuwa amehusika katika mwaliko wa awali wa mimi kuzungumza na wanafunzi.

Alinikaribisha kwa uchangamfu, jambo lililonituliza, kisha akaniambia jinsi alivyowaona wanafunzi wale wale asubuhi ile. “Sijapata kuwaona wakiwa na shauku na hamu kubwa hivyo ya kuzungumza juu ya Mungu,” akasema. “Walishangaa kumkuta mwanasayansi ambaye pia ni mtu wa imani.”

Ni jambo la kusikitisha jinsi gani kwamba watu wengi wana udanganyifu huu. Uzoefu wangu ni kwamba idadi kubwa kiasi ya wanasayansi pia ni watu wa imani kuu. Naam, wengi wangesema kwamba wanamwamini Mungu kwa sababu, kama wanasayansi, wanapaswa kuuliza maswali halisi kuhusu maisha, nao hupata majibu pekee katika kuamini!

Rabi aliendelea, “Kinachonisikitisha ni kwamba wanafunzi wangu wanamwamini Mungu vichwani mwao tu, nami sijui jinsi ya kukiingiza kitu hicho mioyoni mwao!”

Nilimwambia kwamba kuna njia moja tu, nayo ni kukiri kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu, Masihi. Akasema kwamba ingetubidi tukubaliane kutokubaliana, lakini hoja ilikuwa imefikishwa.

(Kwa habari kamili zaidi ya kipindi kile cha ajabu katika Chuo cha Kiebrania, ambako nilipewa uhuru mwingi wa kushiriki imani yangu thabiti juu ya Kristo, soma kitabu changu kingine “Stepping Stones.”)

Ni imani yangu ya kusikitisha, baada ya miaka mingi nikiwa mchungaji, kwamba watu wengi katika makutaniko yetu hawatofautiani na wanafunzi wale Wayahudi. Wana maarifa ya kichwani, lakini hawana uzoefu wa Kristo aliye hai. Wanatumaini (kwa maana ya kidunia, pamoja na uwezekano wake wa kushindwa), lakini hawajui lolote juu ya “Kristo ndani yenu, tumaini la utukufu” (Wakolosai 1:27). Naam, kwa wengi sana, neno ‘uzoefu’ huchochea taswira za hisia zilizopita kiasi na Wakarismatiki wapotovu, nao wamekusudia kujilinda dhidi ya kupita kiasi kwa namna hiyo.

Ni mtume Yohana ‘mpendwa’ aliyeandika, “Mambo hayo nimewaandikia ninyi mnaoliamini (kwa kichwa?) Jina la Mwana wa Mungu; ili mpate kujua (kwa hakika ya ndani?) ya kuwa mna uzima wa milele, tena mpate kuliamini (kwa moyo?) Jina la Mwana wa Mungu” (1 Yohana 5:13).

Katika waraka wake wote anasisitiza mara kwa mara kuipitia imani yetu kwa uzoefu. Anaandika juu ya kushirikiana na Baba na kujua kwamba tunamjua. Tunajua hilo kwa sababu tunauonja upendo wake na Roho wake, akishuhudia pamoja na roho zetu ya kuwa sisi ni wana wa Mungu.

Imani Iokoayo, kipawa kutoka kwa Mungu, hutuwezesha kuugusa uungu, na kufungua mfereji ili uzima uweze kutiririka ndani ya nafsi zetu. Roho Mtakatifu hutia uzima, nasi tunazaliwa mara ya pili. Tunabatizwa na Roho kuingia katika Mwili wa Kristo na kuwa kitu kimoja pamoja na wote walio katika Mwili huo (1 Wakorintho 12:13). Kuamini kwetu kwa kichwa kunakuwa kujua kwa moyo; lakini sisi ni watoto wachanga tu katika imani, nasi tunahitaji kukua.

Tena, ni imani yangu ya kusikitisha kwamba sehemu kubwa ya waaminio waliozaliwa mara ya pili hawaendelei mbali kutoka mahali hapa pa kuanzia. Bado wanahitaji kufundishwa kanuni za Neno la Mungu. Wanahitaji maziwa, wala si chakula kigumu. Hawana ujuzi wa neno la haki, kwa maana wangali watoto wachanga (Waebrania 5:11-14).

Katika waraka wa kwanza wa Yohana, mtume yule mzee anaweka mbele - kile ninachoamini kuwa - kipimo cha ukomavu wa Kikristo. Anawafananisha wasomaji wake na watoto, vijana, na baba (1 Yohana 2:13-14). Ni jambo la kuvutia jinsi anavyowahutubia kila mmoja wa hawa watatu, kwa maana haandikii wale wanaoingia katika makundi hayo kwa kadiri ya umri, bali kiroho. Nimekutana na baadhi ya vijana wa kiume na wa kike ambao Yohana angewaita baba na mama katika imani. Kwa kusikitisha, kinyume chake, nimekutana na waaminio wengi walio wazee zaidi, waliokuwa kanisani kwa miaka kadhaa, lakini hawajapata kuendelea zaidi ya kuwa watoto wasiokomaa.

Yesu alisema kwamba tusipokuwa kama watoto wadogo hatuwezi kuingia katika ufalme wa Mbinguni, lakini tukiisha kuingia kwa njia ya kuzaliwa upya (Yohana 3:3-36), anatarajia tukue hata tufikie ukomavu. Nashangaa jinsi Wakristo wengi walivyo kama watoto wachanga katika kutokomaa kwao.

Watoto wadogo wamesamehewa dhambi zao na wana uhusiano na Baba. Wanaweza kuomba na kufurahia baraka za ushirika, lakini wanaonyesha ushahidi mdogo wa ukuaji wa Kikristo. Mtu wa namna hiyo aweza kuwa wa umri wowote ule, lakini anabaki mtoto mchanga kiroho. Wana imani iokoayo, lakini hawana zaidi ya hapo.

Kijana ni yule ambaye “amemshinda yule mwovu, akiwa na nguvu kwa kuwa neno la Mungu linakaa ndani yake” (1 Yohana 2:14). Wako hai katika vita vya haki; wakienenda katika ushindi, na kuzidi kumjua Mungu katika sifa zake nyingi zaidi.

Waaminio wengi hawatambui kwamba kuna vita vinavyoendelea, nao huishi maisha yao pasipo kuzijua hila za Shetani ambazo huwanyang’anya furaha na ushindi ambao ungekuwa wao. Wengine wanajua kuna vita lakini wanawadhani wapiganao kuwa ni Mungu (au Yesu) na Shetani. Na tuwe wazi juu ya jambo hili - hakuna vita vinavyoendelea leo kati ya Yesu na Shetani - vita hivyo vilipiganwa msalabani miaka 2000 iliyopita na Yesu alishinda!

“Akiisha kuzivua enzi na mamlaka, alizifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo” (Wakolosai 2:15).

Vita vya leo ni kati ya Shetani na sisi. Je, jambo hilo linakutia hofu? Halipaswi kufanya hivyo utakapozitambua hila zake na kujua kwamba Bwana anatarajia ushinde kwa sababu “yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia” (1 Yohana 4:4).

Paulo angeweza kusema kwa haki, “Mimi sina ujinga wa hila zake” (2 Wakorintho 2:11). Ni wangapi kati yetu wawezao kusema vivyo hivyo? Kijana anaweza, “kwa maana ana nguvu, na Neno la Mungu linakaa ndani yake” (1 Yohana 2:14).

Baba ni yule aliyekomaa, aliyepita katika hatua zile nyingine mbili. Amefikia kumjua “yeye aliye tangu mwanzo” (1 Yohana 2:14). Anamjua yule wa milele. Bila shaka hili ndilo lipasalo kuwa lengo letu, “Kumjua yeye na kumfanya ajulikane” (Yohana 17:2 na Mathayo 28:19-20).

Nakumbushwa juu ya Musa aliyejulikana kuwa rafiki wa Mungu. Aliongea na Mungu juu ya Mlima Sinai na ndani ya hema ya kukutania, hata uso wake ukang’aa, na watu wasiweze kuvumilia kuutazama mng’ao wake. Alimjua Mungu kwa undani; lakini kuonja mambo ya kimungu huzaa tu shauku ya kuonja zaidi, na hivyo yule nabii anamwomba Mungu, rafiki yake, ombi.

“Ee Bwana,” analia, “nakuomba unionyeshe utukufu wako!” (Kutoka 33).

Mungu anasema kwamba hawezi kuufunua utukufu wake kwa sababu jambo hilo bila shaka lingesababisha kifo cha Musa; lakini anaongeza neno la kushangaza.

“‘Musa,’ akasema Bwana, ‘Ninalijua jina lako, kwa hiyo nitakufunulia jina langu,’” naye anaendelea kujitangaza kuwa ni Mungu wa rehema na neema, mvumilivu, tena mwingi wa wema na kweli (Kutoka 3:13-15). Katika siku za Biblia, jina la mtu lilieleza tabia yake, kama itakavyoonekana ukifanya uchunguzi wa majina ya Kibiblia.

Mungu anasema kwamba anaijua tabia ya Musa, na kwa hiyo yu tayari kuifunua tabia yake mwenyewe.

Je, wataka kumjua zaidi Mungu, yeye aliye tangu mwanzo, yule wa Milele? Anataka kujifanya ajulikane kwako, naye analijua jina lako!

Awezaje kuifanya tabia yake ijulikane ikiwa jina lako ni ‘asiye mwaminifu’, ‘mnafiki’, ‘mwenye shaka’, ‘mwenye kiburi’, ‘dhaifu’, ‘mdanganyifu’, au ‘mtoto mchanga’?

Anangoja mpaka utakapokua hata ukomavu kama yule kijana ambaye jina lake ni ‘mwenye nguvu’, ‘mshindi’, ‘mwaminifu’, na ‘mtu wa uadilifu’; kisha anajifanya ajulikane zaidi, ili uweze kuendelea kukomaa hata kufikia kimo cha baba au mama wa imani.

Mshukuru Mungu kwa kipawa chake cha ajabu cha imani iokoayo, lakini ni lazima tuendelee mbele hata kufikia ukomavu wa imani.

Tunda la Imani “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria” (Wagalatia 5:22-23).

Tuliponunua nyumba yetu ya kwanza huko Kanada, tulifurahi kwamba kulikuwa na miti kadhaa ya matunda bustanini. Kulikuwa na mti wa tofaa, miti miwili ya plamu na miti miwili ya cheri; lakini tuliishia kukata tamaa majira ya joto yalipofika kwani matunda yalikuwa duni. Niliamua kuipogoa miti, hivyo nikiwa na msumeno mkononi, nikafanya kazi ile. Nilijua kidogo tu juu ya kupogoa miti isipokuwa kwamba ni muhimu kufungua sehemu ya kati ya mti ipate jua, na kuondoa machipukizi yote ya bure ambayo yangenyonya virutubisho vitoavyo uhai kutoka matawi yazaayo matunda.

Rafiki zangu walisema kwamba, katika ujinga wangu wa mbinu sahihi ya kupogoa, nilikuwa nimekata sehemu nyingi mno na sasa miti ile hakika ingekufa. Majira ya joto yaliyofuata tulitazama kwa mshangao kila mmoja wa ile miti ukizaa matunda mengi mazuri kiasi cha kuinama hata chini.

Naikumbuka vyema jioni ile ambayo mimi na Anne tuliketi nje juu ya bembea yetu ya bustanini, tukifurahia hali ya hewa nzuri ya Ontario. Tulisikia sauti ya ajabu, ikafuatiwa upesi na sauti nyingine kama hiyo. Ilikuwa kama kilio kirefu cha kuugua kikifuatwa na “aahhh…” ya ghafula ya faraja. Tulitazama huku na huku kuona kama kuna mtu aliye na maumivu karibu nasi. Fikiria mshangao wetu tulipotambua kwamba sauti ile ilitoka katika miti yetu ya matunda! Kisha tukaona sababu ya kuugua kule.

Mojawapo ya matawi ya mti wetu wa tofaa lilikuwa likivimba na kule kuugua kulionyesha jitihada ya mti ulipokua. Ghafula ikawa sauti ya faraja pale uvimbe ulipopasuka na tofaa likachomoza kuchukua nafasi yake miongoni mwa matunda mengine yote mazuri juu ya tawi lile! Miti yetu ya cheri na plamu ilikuwa ikifanya vivyo hivyo, ingawa kuugua kwake kulikuwa na sauti tofauti.

Ni dhahiri, miti ile ilikuwa ikijitahidi sana kutufurahisha kwa kuzaa matunda bora kadiri iwezavyo!

Bila shaka, hakuna hata mmoja wenu angeiamini hadithi ile. Ni upumbavu kudhani kwamba mti waweza kuzaa matunda kwa jitihada yake mwenyewe! Lakini, hivyo ndivyo hasa waaminio wengi wanavyofikiri linapokuja suala la kuwa na tunda la Roho katika maisha yao! Kwa namna fulani, tunadhani hatuwezi kuwa na tunda la imani isipokuwa tufanye kazi kwa bidii sana ili kulizaa, na kwa kuwa wa kiroho zaidi!

Daudi Mtunga-Zaburi alielewa jinsi tunda la kiroho lizaavyo naye akaandika katika Zaburi 1:3 kwamba “[mtu] mwenye haki atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake.”

Yote afanyayo mti ni kusimama pale tu! Hufungua matawi yake kwa jua, hunywa mvua, na huvuta utomvu wake kutoka ardhi yenye maji iliyo chini yake. Kisha asili ya uhai ulio ndani ya mti huzaa tunda linalofaa. Vivyo hivyo, tunda la kiroho huzaliwa.

Tunapokaa ndani ya mzabibu - ambaye ni Yesu - mioyo yetu hufunguliwa kwa ‘uso ung’aao’ wa Mungu nasi huteka kutoka visima vya Roho wa Mungu. Kisha tunda - sifa za uhai mpya ulio ndani yetu - huzaliwa kwa majira yake. Jambo hili halitokei mara moja usiku mmoja. Huchukua muda kukomaa kama Mkristo, huhitaji utayari wa kupogolewa, huhitaji kusimama juu ya ahadi za Neno la Mungu, tena huhitaji kutumaini kwa kuendelea. Halihitaji jitihada!

Waaminio wengi hujiona kama miti, lakini hutumia muda mwingi kujichunguza wenyewe kutafuta ushahidi wa tunda. Badala ya kutazama kotekote katika ‘matawi’ kuona kama tunda linaonekana, tungekuwa tumejishughulisha vyema zaidi kwa kuyageuza macho yetu kuelekea shina la mti, chanzo cha lishe yote wanayoipokea matawi. Ingekuwa afadhali tuyaelekeze macho yetu kwa Yesu, mzabibu wa kweli ambao ndani yake tumepandikizwa. Ndipo tunda lingekua, na wengine wangeliona kwa majira yake.

Ni yeye azaaye tunda la imani ndani ya wote wanaokaa ndani yake na, kama ule mti wa Zaburi 1, wateka kutoka vijito vya maji ya Roho Mtakatifu.

Na tuelewe jambo lingine zaidi juu ya tunda lote la Roho. Kwa urahisi sana tunalihusianisha na sifa zinazopatikana kwa watu wote, lakini linapatikana tu kwa wale waliozaliwa mara ya pili na Roho. Ni yeye azaaye tunda hilo ndani yetu, na yeye asiye Mkristo hawezi kujua lolote juu yake!

“Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni” (1 Wakorintho 2:14).

Hivyo basi, uvumilivu kwa mfano, hauhusiani sana na kusubiri kwa saburi taa za barabarani zibadilike! Wengi wasioamini wana uvumilivu mwingi kuliko waaminio! Ulimwengu hauwezi kujua lolote juu ya upendo ule uliomiminwa katika moyo wa mwamini, furaha ile idumuyo wakati kila kitu kinachotuzunguka kinakwenda vibaya, amani ile iliyo katikati ya dhoruba. Hivi ni tunda la Roho akaaye ndani, tena ni utajiri kwa mtoto wa Mungu peke yake.

Vivyo hivyo, tunda la imani litaonekana tu katika maisha ya mwamini anayekomaa.

Ninapozichunguza matunda haya tisa, nimefikia maoni kwamba yanazidi kuwa ya kigeni au adimu kadiri ninavyoendelea kusoma. Kila mwamini mpya amekwisha kuonja kiasi fulani cha upendo, furaha na amani. Kweli, tangu wakati wa kuzaliwa upya, wengi wanaweza kushuhudia kwamba, “mbingu juu ni buluu laini zaidi, dunia pande zote ni kijani tamu zaidi; kuna kitu kiishicho katika kila rangi ambacho macho yasiyomjua Kristo hayajapata kukiona” (G Wade Robinson).

Kisha, muda uendeleapo, ile furaha na amani ya awali huonekana kutoweka Baba anapoanza mchakato wa kutuadibisha ili kutufananisha na sura ya Mwanawe; lakini tunapokaa ndani yake, tunda hurudi katika uzoefu ulio na utajiri na ukamilifu zaidi. Awali tuliuonja upendo wake ukitulemea, lakini sasa twaukuta ukiwafikia wengine kupitia sisi. Furaha yake ilikuja kwanza kama wimbo mpya mioyoni mwetu ukifanya maisha yaonekane kama siku mpya, lakini sasa twaanza kuukuta wimbo huo ukibubujika ndani yetu hata katika usiku ulio na giza kuu kabisa.

Mwanzoni, amani yake ilizituliza dhoruba zilizokuwa zikivuma mioyoni mwetu, lakini sasa amani yake ni usalama wa ndani sana katikati ya dhoruba za maisha.

Katika mwamini anayekomaa, twaanza kuona zaidi tabia ya Yesu katika kuvumilia dhihaka za ulimwengu. Uvumilivu wetu huchukua nafasi ya asili ya uasi ya yule mtu wa kale tuliokuwa zamani, nasi twajikuta hatuitikii hali za majaribu kama zamani.

Imesemwa kwamba ukitaka kuona upole wa Yesu, tazama matendo yake; ukitaka kuona wema wake, tazama mielekeo yake. Hivyo ndivyo ilivyo kwamba, tunapokua katika tunda la Roho, twakomaa katika matendo yetu na mielekeo yetu vilevile.

Kisha maisha ya imani hudhihirika mwamini anapoanza kuenenda katika utii kwa misukumo ya Roho, akiuona mkono wa Bwana ukimwongoza na kumsukuma. Mtu mnyenyekevu ni yule aliyeachilia haki zake mwenyewe na kujisalimisha kikamilifu kwa mapenzi ya Bwana. Yeye ni mwepesi kufinyangwa na kufundishika; anayeweza kufinyangwa kuwa chombo kifaacho matumizi ya mfalme.

Mwishowe, tunda lililo adimu kuliko yote laweza kuja. Hili ndilo tunda ambalo mtume Paulo alilitamani: kiasi. Huku ndiko ‘kufisha’ alikoandika juu yake katika Warumi 7:15-24. Alitambua jinsi ambavyo ingekuwa vigumu kwake kuzaa ushindi huu juu ya nafsi kama si kwa sababu, kwa njia ya kazi ya msalaba, kuna ushindi wa namna hiyo uwezekanao.

“Sasa basi hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imekuacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti” (Warumi 8:1-2).

Tunda kama hilo hutoka tu kwa Roho Mtakatifu aliye ndani ya mwamini na vivyo hivyo ndivyo ilivyo kwa imani. Yeye peke yake ndiye awezaye kulizaa; hakuna jitihada yangu itakayofaa!

Ningependa kuweka mbele wazo la ziada juu ya tunda la Roho.

Neno “tunda” liko katika umoja. Haya si matunda mengi mbalimbali yanayokua kila moja peke yake, bali ni tunda moja lidhihirikalo kwa njia tofauti. Imependekezwa kwamba matatu ya kwanza (upendo, furaha, na amani), ni uzoefu wa ndani wa Roho Mtakatifu akaaye ndani ya mwamini, ambapo utatu wa pili (uvumilivu, upole, wema) ni udhihirisho wa nje tunapohusiana na wanadamu wanaotuzunguka, na ule utatu wa mwisho (uaminifu, upole, na kiasi) unahusu muungano wetu na Mungu.

Kipawa cha Imani “Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana… na mwingine imani katika Roho yeye yule…” (1 Wakorintho 12:7, 9).

Aina ya tatu ya imani niipatayo katika Biblia inaitwa kipawa cha imani. Mtume Paulo anaandikia kanisa lililoko Korintho juu ya “charismata”, (ambayo hutafsiriwa kama “vipawa vya neema” kutoka lugha ya Kiyunani) vipawa vitolewavyo na Roho Mtakatifu kwa kanisa. Kuna vipawa vingi vya namna hiyo vilivyoorodheshwa kwa ajili yetu katika Warumi 12 na 1 Wakorintho 12, pamoja na vipawa vya huduma vilivyotajwa katika Waefeso 4:11.

Vipawa hupewa watu binafsi, si ili wapate kujisifu au kujivuna kwavyo, bali ili viwe kwa faida ya wote. Kwa kweli, vipawa hupewa kanisa, na watu binafsi ni vyombo tu ambavyo Roho angevitumia. Ni jambo la kushangaza kwamba katika marejeo yote matatu yaliyotajwa, Paulo pia anasisitiza umoja wa Mwili wa Kristo. Kusudi la vipawa vyote ni kuliwezesha kanisa kukua katika umoja ili lipate kufanikiwa katika huduma yake ya kuwaleta wanaume na wanawake kwa Bwana.

Basi kipawa cha imani hudhihirikaje kikifanya kazi?

Wazia mazingira haya katika kikao cha Halmashauri ya Wazee wa kanisa la mtaa fulani. Pendekezo limetolewa punde tu la kuanzisha kazi ya kuenea katika jirani ili kujaribu kuwafikia vijana wa jamii wasiohudhuria kanisa. Inakubaliwa kwamba hili ndilo kanisa pekee la kiinjili katika eneo lile na kuna idadi inayoongezeka ya vijana, wasio na ajira na wenye uhitaji, wakiunda vikundi vya urafiki.

Waumini wengi wa kanisa wameeleza hisia zao, kuanzia huruma hadi hofu, hivyo pendekezo limetolewa.

Wala mchungaji wala mmoja wa wazee hana nguvu au uwezo wa kufanya kazi na vijana hawa hivyo inatambulika kwamba mfanyakazi mpya wa vijana anahitaji kuajiriwa. “Lakini tutamlipaje na kuigharimia huduma hii?”

Swali hilo ni la dhati kwani kanisa limekuwa likihangaika kifedha katika miaka ya karibuni. Jibu rahisi, na daima yupo mtu atakayelitoa, ni kwamba ‘ni lazima tuombe zaidi, na Mungu atatutimizia.’ Hilo ni kweli maadamu ni kusudi la Mungu kuianzisha kazi na kumwajiri mfanyakazi wa vijana. Lakini twajuaje kama hili ni kusudi lake? Linasikika vizuri, lakini kuna mipango mingi isikikayo vizuri kwetu lakini kamwe haionekani kupokea baraka ya Mungu.

Wazee wanaamua kulingoja jambo hilo, kuomba na kukutana pamoja juma moja baadaye ili kufanya uamuzi.

Wanapoingia katika Chumba cha Halmashauri, wazia wewe ni shahidi asiyeonekana uwezaye kusoma mawazo yaliyo katika akili ya kila mtu. “Mmoja anakubali, mmoja anakataa… wawili wanakubali, watatu wanakubali, wawili wanakataa… wanne wanakubali, wanne wanakataa… na mchungaji…” Watawezaje kabisa kufikia mapatano yoyote wakati vijana walio mitaani wanaendelea katika upotevu wao?!

Wanaume wale wanaanza kwa maombi kisha wanaanza kushiriki mawazo yao. Ghafula, mtu mmoja, aliyeingia akiwa ‘anayekataa’, anasema. “Nilipoingia humu usiku huu, nilikuwa na maoni kwamba huu si wakati wa kuanzisha kazi mpya; lakini, nilipoyasikiliza mabishano ya kuunga mkono na ya kupinga, jambo fulani limetokea ndani yangu nami nimebadili msimamo wangu! Najua kwamba Bwana yumo katika jambo hili! Nampigia kura kwamba tumteue mfanyakazi mpya wa vijana!” Wengine wanaanza kusema, na, ndani ya dakika chache tu, uamuzi wa kauli moja unafikiwa. Nini kilichotokea?

Si kwamba tu kila mtu alisikia yale wengine waliokuwa wakisema bali, kwa sababu walikuwa wanaume waliokuwa wakiyatafuta kwa dhati mapenzi ya Mungu, walimsikia akinena katika roho zao. Alipanda ndani ya kila mmoja wao imani ya kuamini. Hicho ndicho kipawa cha imani.

Ingawa matatizo ya kifedha yalikuwa halisi, aliwapa imani iliyozishinda hali zile. Yaweza kuwa ilikuwa ‘punje ya haradali’ tu (Marko 4:30-32), lakini kwa sababu ilipandwa katika roho zao na Mungu mwenyewe, mlima wao ungeondolewa. Imani ya namna hiyo daima hulipwa thawabu kwa baraka ya Mungu. Imani ya namna hiyo daima huiondoa milima!

Nimeona kipawa cha imani kikifanya kazi mara kadhaa. Nimewaona watu wakifanya mambo makuu kwa ajili ya Mungu wakati wote waliowazunguka waliona haliwezekani. Waliacha kuzitazama hali kwa sababu waliujua msukumo wake.

Nilikuwa na rafiki mpendwa aliyeitwa Yorrie Richards ambaye wakati mmoja alikuwa akigugumia vibaya sana hata ilikuwa haiwezekani kwake kusema sentensi rahisi. Alikuja kumjua Bwana alipokuwa akikabili kesi ya mahakama kwa wizi. Hakimu wa kesi ile alimwonya kwamba “njia uliyoichagua kuifuata yaweza kuishia kwenye mti wa kunyongea”. Mji wote ulijua historia yake ya uhalifu, na wengi walikuwa na mashaka juu ya wongofu wake.

Muda fulani baadaye, mimi na Yorrie tulikutana tena naye akanipendekezea jambo lililo gumu kuliko yote. Alitaka kukodi ukumbi mkuu katika mji wake wa nyumbani na kuihubiri injili kwa wote waliokuwa wamemjua katika ujana wake nao walikuwa wasioamini kabisa. Nilimshauri asifanye ujasiri wa namna hiyo kwani bila shaka ungetusababishia aibu kubwa na kwa vigumu ungeweza kuifaidi injili kwa jambo lolote. Alisisitiza kwamba Bwana alikuwa amemwekea jambo hili moyoni mwake, naye aliamini kuwa ndiyo mwongozo wake.

Tulikodi ukumbi na kutangaza mkutano. Nilisimama kando baada ya utangulizi na Yorrie akawakabili wasikilizaji wake. Mara moja akaanza kugugumia, nami nikahisi aibu kwa ajili yake. Sikuweza kabisa kujilazimisha kusikiliza.

Kisha ukimya wa ajabu ukatanda chumbani sauti ya Yorrie ilipozidi kudhibitika naye akaanza kunena kwa mamlaka na ujasiri, akihadithia yale Bwana aliyoyatenda. Machozi mengi yalidondoshwa usiku ule Mungu alipofanya muujiza miongoni mwetu, kwa sababu mmoja wa wale ‘wanyonge na wapumbavu’ wake alikuwa amekiitikia kipawa chake cha imani. Maelfu mengi kotekote Uingereza na Kanada wanaweza kushuhudia leo juu ya mahubiri yaliyotiwa mafuta ya Yorrie Richards.

Hivyo, nawaletea aina tatu za imani: imani iokoayo, tunda la imani, na kipawa cha imani.

Kinachonigusa mara moja ni kwamba zote tatu hupata chanzo chake katika Mungu, si katika mwamini! Hakuna lolote niwezalo kufanya ili kuzaa imani ndani yangu, hivyo tafadhali usiniambie ‘uwe na imani zaidi’ unaponiona nikiwa mgonjwa au nikihangaika katika mwenendo wangu wa Kikristo. Kile ninachohitaji kukikuza ni kutumaini zaidi, si imani.

Ukurasa 1 / 14 · 19 dakika zimebaki katika sura
Ochorus

Kuwawezesha watu vitabu vya Kikristo vya kale — bila malipo, kwa lugha yako.

Chunguza

Dhamira Yetu

Vitabu vya Kikristo vya kale bila malipo mtandaoni — na vitabu vilivyochapishwa tunavyogawa kwenye makongamano, makanisa, shule na magereza kote Afrika Mashariki.

Faragha na Masharti

Huduma tangu 2021 · Victoria BC, Kanada · Kampala, Uganda