Sura 15 · dakika 6 za kusoma

Yusufu

«Kwa imani Yusufu, hapo alipokuwa akifa, alitaja habari ya kutoka kwao wana wa Israeli; akaagiza mambo ya mifupa yake» (Waebrania 11:22).

Habari fupi ya jinsi Yusufu alivyowasamehe ndugu zake waliokuwa wamemtenda vibaya sana inapatikana mwishoni mwa Mwanzo 50. Hapo twapata kauli ile ya ajabu, «Ninyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia yawe mema, ili kutimiza mambo yaliyoko leo, na kuokoa uhai wa watu wengi» (Mwanzo 50:20). Ingawa mara nyingi adui huwaletea watu wa Mungu mashambulizi, Baba yetu aweza kuyageuza yawe mema, kwa faida yetu na kwa heshima ya jina lake.

Inashangaza kwamba mwandishi wa Waebrania hakuyataja mabonde na milima ambayo kwayo na juu yake Yahweh alimwongoza Yusufu alipoandika habari za imani, bali badala yake alichagua jambo lionekanalo dogo lifungalo kitabu cha kwanza cha Biblia.

«Mimi ninakufa; lakini Mungu atawajilia bila shaka, naye atawapandisha kutoka nchi hii mpaka nchi ile aliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo» (Mwanzo 50:24). Kisha akawaapisha ndugu zake ya kwamba Mungu atakapowajia, watachukua mifupa yake pamoja nao mpaka nchi ile iliyoahidiwa.

Ingekuwa miaka mingine 400 kabla ya unabii huu wa Yusufu kutimia chini ya uongozi wa Musa. Kwa habari ya utimilifu wa ombi lake tazama Kutoka 13:19 na Yoshua 24:32.

Yusufu alikuwa na ufunuo wa ndani uliotoka kwa Mungu, ambao aliukiri kwa kinywa chake, kama vile mtume Petro angefanya juu ya Mlima.

Hermoni, zaidi ya miaka 2000 baadaye. Humo ndimo imani yake ilipo.

Twaweza kujifunza nini kutokana na mstari huu?

Kwanza, twaona kufanana kati ya hali yake na hali ya baba yake na babu yake. Kama Isaka na Yakobo, yeye alikuwa mgeni, msafiri katika nchi ya ugenini. Watu hawa watatu wote walikufa bila kuingia katika ile ahadi Mungu aliyoifanya, ahadi ya nchi iliyoahidiwa na ya ukuu wa taifa la Israeli. Isaka alibaki mhamiaji na mtangatanga, Yakobo alikuwa bado uhamishoni katika nchi ya Misri, naye Yusufu alikuwa amefikia vilele vya juu vya utukufu, lakini bado ulikuwa ukuu wa mgeni katika nchi ya ugenini. Lakini kwa wote watatu, Mungu aliwapa ushuhuda ya kwamba ahadi yake haitaanguka. Walikufa katika tumaini, si katika kukata tamaa.

Hali yetu maishani iwe vyovyote, tumeitwa kuiendea njia ile ile waliyoiendea mababa hawa: njia ya imani. Sisi pia twaweza kupanda hadi kwenye utukufu katika ulimwengu huu, lakini kamwe tusisahau ya kuwa sisi ni raia wa ufalme mwingine, ulio wa juu zaidi. Wengi wetu hawatapata kamwe kuonja ahadi kubwa zaidi za Mungu, lakini kila mmoja wetu lazima aishi kwa jinsi ambayo itasogeza karibu ile siku ambayo wengine wataweza kuzifurahia. Yesu alitoa ahadi ya ajabu ya kwamba Injili lazima ihubiriwe katika ulimwengu wote kwa mataifa yote «ndipo ule mwisho utakapokuja» (Mathayo 24:14). Mwishowe atakomesha dhambi na kuuleta ufalme wake wa haki.

Uishipo katika ulimwengu leo, waweza kuamini ya kuwa kuja kwake bado ni mbali sana. Hata hivyo, mfano wa Yusufu umetolewa ili kutufundisha ya kwamba yatupasa kuutazamia mbele daima uhakika wa kutimizwa kwa ahadi, na kuishi maisha ya kutarajia namna hiyo. Yatupasa kuishi kila siku katika nuru ya umilele.

Kwa miaka mingi Yusufu alikuja kuufahamu uaminifu wa Mungu, na maneno yake yakabadilika. Hakusema tena juu ya ndoto ambazo katika hizo angeitawala jamaa yake. Hakusema, «Nendeni mkamwambie baba yangu habari za utukufu wangu wote katika Misri.»

Mwandishi wa Waebrania ameuchagua mfano wa siku zake za kufa ili kutufundisha jambo fulani. Yusufu anakaribia mwisho wa utukufu wake wa kidunia, naye ametambua ya kuwa fahari na heshima zote za ulimwengu huu si kitu kwa mtu anayekufa. Zaweza kuridhisha kwa kitambo, lakini mwishoni ni kama povu lipasukalo.

Uhai ni kitu kipitacho upesi.

«Uzima wenu ni nini?» asema Yakobo, «Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka» (Yakobo 4:14).

Mungu anaichochea imani ndani ya yule mzee hata sasa anaona ulipo urithi wake wa kweli. Uko katika nchi ijayo na katika kuja kwa mkombozi ajaye. Mtu angedhani ya kwamba angetaka wazao wake wabaki katika nchi hii ya Misri iliyomtendea mema hivyo. Kwa nini basi hataki mwili wake ubaki humo? Labda kama asingezikwa katika Misri wangemjengea ukumbusho mkuu, kaburi kubwa mahali paonekanapo, au huenda wangeliita jengo kuu kwa jina lake; jina lake lingejulikana milele. Naam, angeweza kujengewa hekalu kwa ajili ya Yahweh na kuliita «Kanisa la Ukumbusho la Yusufu benYakobo wa Kwanza.» Kwa njia hiyo angeweza kumletea Mungu heshima bila kupoteza chochote cha utukufu wake mwenyewe!

Lakini Mungu hatashiriki utukufu wake na mwanadamu, wala na kiumbe chake chochote. Bila shaka ninadhihaki, lakini je, si jambo la ajabu jinsi wengi wa 'watu wa Mungu' mashuhuri wa siku zetu wamekazania kwa ung'ang'anizi utukufu au sifa yao inapokuwa hatarini katika vita vya uadilifu na uaminifu kwa kazi ya Mungu? Je, si jambo la ajabu jinsi waaminio waweza kuvutwa kwa urahisi 'kuifanya kazi hii' au 'kutoa kwa ajili ya jambo lile,' pale zilipo thawabu au umaarufu vinavyohusiana navyo? Badala yake, tumeitwa kuwa kama watu waliokufa, wasiodai haki zao wenyewe wala kutafuta umaarufu katika ulimwengu huu. Mungu hakutuita tuwe mashuhuri au wenye kufaulu; ametuita tuwe waaminifu.

Kama Yusufu, dhamira yetu inapaswa kuwa kuja kwa mkombozi wetu na kukusanywa kwetu pamoja kwake. Yesu ndiye mkombozi wetu, naye anakuja upesi. Ameshatukomboa kutoka adhabu ya dhambi - kuhesabiwa haki, ukamilifu wa roho zetu. Sasa anatukomboa kutoka nguvu ya dhambi - utakaso, ukamilifu wa nafsi zetu, naye atakuja upesi kutukomboa kutoka uwepo wa dhambi - kutukuzwa, ukamilifu wa miili yetu!

Nina hakika ya kwamba, tofauti na Yusufu, hatuna budi kungoja zaidi ya miaka 400, bali ya kuwa «karibu, karibu sana, tutamwona Mfalme» (Andraé Crouch, Soon and Very Soon). Nionapo ulimwengu huu pamoja na matatizo yake yanayozidi ya wingi wa watu uliopita kiasi, njaa, majanga ya asili, na kuvunjika kwa jamaa na mifumo ya kijamii. Nilitazamapo kanisa pamoja na kuenea kwake kukubwa na programu za umisionari katika sehemu nyingi za ulimwengu, nina hakika ya kuwa anakuja upesi. Niutafakaripo mgawanyiko ndani ya kanisa kati ya wale walio waaminifu kwa Neno lake na wanachama wake walio na msimamo huru zaidi, sikati tamaa, bali natambua ya kuwa sasa anamwandaa na kumtakasa bibi-arusi wake. Tukiwa hai atakapokuja, tutakwenda katika urithi ule, lakini tukilala, hatutaachwa nyuma. Basi, katika maneno ya Yusufu aliyoyanena kwa imani, twawaona walio hai na waliokufa wakienda pamoja kutoka mahali pa utumwa.

«Waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele» (1 Wathesalonike 4:16-17).

Hakika fahari na uzuri wa bandia wa ulimwengu huu unafifia tunapoitazamia mbele siku ile ya furaha, itakayotokea karibu hivi. Je, twaifanya hii kuwa dhamira yetu ya kila siku? Labda twahitaji kurudi tena kwenye 'kitanda chetu cha kufa' chini ya msalaba ambapo maono yetu yatabadilika, kwa sababu watu waliokufa hawayajali mambo ya ulimwengu huu.

Muhtasari Alipokuwa katika kitanda chake cha kufa, Yusufu alipewa imani ya kutazama mbele katika wakati ujao na kumwona yule mkombozi, Musa, ambaye angekuja kuwaongoza watu wa Mungu kutoka Misri na kuwapeleka katika urithi wao.

Ingawa alikuwa mtu aliyefaulu katika Misri, imani ilidhihirisha ya kuwa kulikuwa na nchi iliyo bora na wakati ujao ulio bora kwa ajili ya wana wa Israeli.

1. Mkombozi, Yesu, amekuja kutuchukua kutoka utumwa wetu na kutuongoza mpaka ufalme wake ulioahidiwa.

2. Imani hutufanya tutazame mbele kwa macho ya watu waliokufa kwa ulimwengu huu.

3. Hatima yetu haipatikani katika mali au cheo chetu - inapatikana katika ahadi yake.

4. Yatupasa kuishi kila siku katika nuru ya kuja kwake mara ya pili.

5. Maisha haya ni kitambo kipitacho tu.

Ukurasa 1 / 5 · 6 dakika zimebaki katika sura
Ochorus

Kuwawezesha watu vitabu vya Kikristo vya kale — bila malipo, kwa lugha yako.

Chunguza

Dhamira Yetu

Vitabu vya Kikristo vya kale bila malipo mtandaoni — na vitabu vilivyochapishwa tunavyogawa kwenye makongamano, makanisa, shule na magereza kote Afrika Mashariki.

Faragha na Masharti

Huduma tangu 2021 · Victoria BC, Kanada · Kampala, Uganda