Sura 6 · dakika 5 za kusoma
Musa, Mtu wa Mungu
Hii ndiyo baraka ambayo Musa, mtu wa Mungu, aliwabariki wana wa Israeli kabla ya kufa kwake—Kumbukumbu la Torati 33:1. Mtu wa Mungu! Jina hilo lamaanisha mengi kiasi gani! Mtu atokaye kwa Mungu, aliyechaguliwa na kutumwa naye. Mtu aendaye na Mungu, aishiye katika ushirika wake na kubeba alama ya uwepo wake. Mtu aishiye kwa ajili ya Mungu na mapenzi yake; ambaye nafsi yake yote imejaa na kutawaliwa na utukufu wa Mungu; ambaye bila kukusudia na bila kukoma huwaongoza watu wamfikirie Mungu. Mtu ambaye moyoni na maishani mwake Mungu amechukua nafasi ipasayo kuwa Yote katika Yote, na aliye na shauku moja tu, kwamba Mungu apate nafasi hiyo katika ulimwengu wote.
Watu wa Mungu kama hao ndio ulimwengu unaowahitaji; ndio Mungu awatafutao, ili awajaze Yeye Mwenyewe, na kuwatuma ulimwenguni kuwasaidia wengine wamjue. Musa alikuwa wa pekee hivi hata watu waliongea juu yake kwa asili hivi—Musa, mtu wa Mungu! Mtu kama huyo ndicho kila mtumishi wa Mungu apaswacho kulenga kuwa—shahidi aliye hai na uthibitisho wa Mungu alivyo kwake mbinguni, na alivyo kwake duniani, na kile anachodai kuwa katika yote.
Katika sura iliyotangulia, tulizungumza juu ya umoja na Mungu kama kile mwanadamu alichoumbiwa, kama pendeleo la maisha ya kila siku, kama kile kilichopaswa kuwa hangaiko letu la kwanza katika zamu ya asubuhi. Kile kilichokuwapo hasa kilihusu uhitaji wetu binafsi, na nguvu ya maisha ya kimungu yenye furaha yaathiriyo wengine. Jina, Musa mtu wa Mungu, na wazo la mtu kuunganishwa kwa karibu na waziwazi na Mungu hivi hata watu kwa silika walitoa hilo kuwa sifa yake kuu—mtu wa Mungu, linatuongoza mbali zaidi.
Linatutoa nje katika maisha ya hadhara, linaonyesha wazo la athari tumfanyayo watu, na nguvu tuwezayo kuwa nayo ya kubeba alama ya uwepo mtakatifu wa Mungu pamoja nasi, hata watu wanapotuona au kutufikiria, jina lije mara moja moyoni—MTU WA MUNGU! Hawa ndio watu ambao ulimwengu na Mungu vyote vinawahitaji sawasawa. Na kwa nini? Kwa sababu ulimwengu, kwa dhambi, umeanguka mbali na Mungu. Kwa sababu katika Kristo ulimwengu umekombolewa kwa ajili ya Mungu. Na kwa sababu Mungu hana njia ya kuwaonyesha watu wanachopaswa kuwa, ya kuwaamsha na kuwaita na kuwasaidia, ila kwa njia ya watu wa Mungu, ambao ndani yao uzima wake, Roho wake, nguvu zake vinafanya kazi.
Mwanadamu aliumbwa kwa ajili ya Mungu, ili Mungu apate kuishi, kukaa, kufanya kazi, na kudhihirisha utukufu wake ndani yake na kupitia yeye. Mungu angekuwa yote katika yote kwake. Ukaaji wa Mungu ndani ungekuwa wa asili na wa kufurahisha kama ulivyo wa kweli, wa ajabu, na usioeleweka. Ukombozi wa Kristo ulipokamilishwa katika kushuka kwa Mungu, yaani Roho Mtakatifu, mioyoni mwa watu, ukaaji huu wa ndani ulirejeshwa, na Mungu akapata tena kumiliki makao yake.
Hapa ndipo mtu ajitoapo kabisa kwa uwepo wa Roho Mtakatifu, si tu kama nguvu ifanyayo kazi ndani yake bali kama Mungu akaaye ndani yake (Yohana 14:16, 14:20, 14:23; 1 Yohana 4), aweza kuwa, katika maana ya ndani kabisa ya neno, MTU WA MUNGU! Paulo anatuambia kwamba ni kwa nguvu ya Maandiko Matakatifu kwamba “mtu wa Mungu awe kamili.”
“Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” Hili latuleta kwenye faida ya zamu ya asubuhi kama wakati mkuu wa kujifunza Biblia binafsi. Ni kadiri tunavyoutoa moyo na maisha kwa Neno, ili Mungu kwa njia ya mafundisho yake, karipio lake, kunyoosha kwake, na maagizo yake achunguze na kuunda maisha yetu yote, na hivyo tunapokuja chini ya utendaji wa moja kwa moja wa Mungu, na katika umoja kamili naye, kwamba mtu wa Mungu atakuwa kamili—amekamilishwa kwa kila tendo jema.
Ee! Kupata neema ya kuwa kweli mtu wa Mungu! Mtu ajuaye na kudhihirisha mambo haya matatu: Mungu ni yote; Mungu adai yote; Mungu afanya yote. Mtu aliyeona nafasi Mungu aliyonayo katika ulimwengu wake na katika watu—Yeye ni Yote katika Yote! Mtu aliyefahamu kwamba Mungu adai na lazima awe na yote, na aishiye tu kumpa Mungu haki yake na utukufu wake! Mtu aliyegundua siri ile kuu kwamba Mungu afanya yote, na atafutaye, kama Mwana wa Mungu, kuishi katika ule utegemezi wa baraka usiokoma kwamba Baba aliye ndani yake anena maneno na kufanya kazi.
Ndugu! Tafuta kuwa mtu wa Mungu! Katika zamu ya asubuhi, Mungu awe yote kwako. Wakati wa mchana, Mungu awe yote kwako. Na maisha yako yajitoe kwa jambo moja, kuwaleta watu kwa Mungu, na Mungu kwa watu, ili katika Kanisa lake, na katika ulimwengu, Mungu apate nafasi imstahiliyo.
“Kama mimi ni mtu wa Mungu, moto na ushuke kutoka mbinguni.” Hivyo ndivyo Eliya alivyojibu jemadari alipomwita ashuke. Mungu wa kweli ni Mungu ajibuye kwa moto, na mtu wa Mungu wa kweli ni yeye ajuaye jinsi ya kuuteremsha moto, kwa sababu ana nguvu kwa Mungu wa Mbinguni. Moto uwe ni ule wa hukumu au wa Roho Mtakatifu, kazi ya mtu wa Mungu ni kuuteremsha moto duniani. Kile ulimwengu unachohitaji ni mtu wa Mungu ajuaye nguvu ya Mungu, na nguvu yake mwenyewe kwa Mungu.
Amini kwamba ni katika desturi ya maombi ya siri ya maisha ya kila siku ambayo hapo twajifunza kumjua Mungu wetu, na moto wake, na nguvu yetu kwake. Ee! Kujua maana ya kuwa mtu wa Mungu, na kile linachomaanisha.
Katika Eliya kama katika Musa, twaona jinsi kunavyomaanisha tu kujitenga na kila maslahi jingine, kujitambulisha kabisa na heshima ya Mungu, si tena mtu wa ulimwengu, bali mtu wa Mungu. Kuna hisi ya siri kwamba haya yote yaleta jitihada na dhabihu, ugumu na hatari, zaidi ya tulivyo tayari. Hili ni kweli tu maadamu hatujaona jinsi dai la Mungu lilivyo kamili, jinsi ilivyo baraka isiyoelezeka kujisalimisha kwake, na jinsi ilivyo hakika kwamba Mungu Mwenyewe atalifanya ndani yetu.
Rudi sasa uangalie Musa, mtu wa maombi, Musa mtu wa ulimwengu, na uone jinsi kutoka humo ilivyoota—Musa, mtu wa Mungu. Ona vivyo hivyo katika maisha ya Eliya—maelewano kati ya kusikia kwetu neno la Mungu na kusikia kwake maombi yetu, na jinsi kwayo inavyokuwa yawezekana kimungu kuwa na kuishi—MTU WA MUNGU. Na kisha uchunguze utumizi wake.